Monday, March 17, 2014

NANI ASIYEGUSWA NA SIASA?

Kwa ufupi hakuna mtu  anayeweza kukwepa kuathiriwa au kuguswa na masuala ya uongozi. Haijalishi unafanya kazi halali au haramu huwezi kukwepa athari za siasa. Unaipenda nchi yako au huipendi siasa na masuala ya uongozi wa nchi yako una sehemu kubwa katika kujenga mazingira ya nchi yako. 


Tunayo mifano mingi ya nchi na mataifa mbalimbali yenye vita na machafuko ya kivita. Tunaona matokeo yake wazi kabisa. Wapo wanawake, watoto, wazee na hata vijana wanaoteseka na hata kufa au kuuawa. Wengine hupoteza makazi yao na kulazimika kuishi katika vichaka na mahema huku wakikabiliwa na  ukosefu wa chakula na maji pamoja na huduma nyingine za kijamii. 

Wengine hufa kwa magonjwa kunakosababishwa na mazingira hatarishi na ukosefu wa huduma za afya na madawa. Swali la kujiuliza ni Je, hao wanaokumbwa na hayo walipenda hivyo?

Fikiri juu mtoto anayekufa kwa sababu ya njaa nchini Sudani ya kusini eti kwa sababu ya vita.
Haijalishi wewe ni nani, haijalishi unafanya nini au unamiliki nini, linapokuja suala la siasa kumbuka una wajibu wa kufanya. Kila mtu katika Taifa lake ana wajibu fulani juu ya siasa ya Taifa lake. Ni kukosa tu uelewa au ni kukata tamaa ndiko kunakowafanya watanzania na hata waafrika kwa ujumla kusema, hawajihusishi na siasa. Haijalishi unajihusisha au la, siasa hugusa maisha yako ya kila siku. Yaani hapa haina haja ya kujua kama wewe unawajibika katika masuala ya siasa ya nchi yako au la, siasa itakugusa tu. 

Inawezekana nisikueleze wajibu wako binafsi hasa ila ukweli usiopingika ni kwamba, wewe una wajibu katika siasa. Kila mtu analo kusudi lililosababisha kuzaliwa au kuishi katika Taifa ulilozaliwa au unaloishi. Ikiwa unaishi katika Taifa lako, katika Taifa ulipozaliwa ni vema kuchukua nafasi yako ya kulitumikia Taifa lako pasi na shaka wala hofu. Tekeleza wajibu wako, fanya likupasalo kufanya kwa maslahi ya Taifa lako.

Kwa hiyo hakuna mtu hata mmoja asiyehusika na uongozi au siasa. Wapo baadhi ya watu wanaodhani kuwa siasa haiwahusu. Uongozi unamhusu kila mtu bila kujali dini, kabila au rangi ya ngozi yake. Mfumo wa uongozi au utawala kwa sehemu kubwa unachangia kujenga au kubomoa maisha ya watu wake kwa namna moja au nyingine. Na wakati mwingine uongozi unaweza kujenga watu wa tabaka fulani na kubomoa au kuathiri vibaya maisha ya tabaka jingine. 

Kwa hiyo usishangae mtu akisema nafasi iliyopo kati ya tabaka la walionacho na wasionacho inazidi kuongezeka katika uongozi huu ukilinganisha na uongozi uliopita. Mfumo wa uongozi au utawala unaweza hujenga misingi ya maisha ya Taifa na unaweza kuiharibu na kujenga misingi mingine isiyofaa. 

Pamoja na uongozi au utawala kuwa na uwezo mkubwa wa kujenga au kuharibu mifumo fulani ya Taifa lakini wananchi wake kwa ujumla wao wana nafasi kubwa ya kukubali au kukataa mfumo wasioutaka. Kwa hiyo binafsi sipendi kulaumu tu uongozi au utawala japo una sehemu yake ya kuwajibika ila wananchi wenyewe wana nafasi ya kuhakikisha wanajenga mfumo wananoutaka wao wenyewe. 

Na hapa ndipo ile dhana ya kulaumu huwa inakufa. Maana huna sababu ya kulaumu mtu mwingine wakati wewe mwenyewe una uwezo na unaweza kusababisha unayoyataka yatokee. Wananchi katika nchi yoyote duniani siku zote wana uwezo wa kusababisha wanayoyataka yatokee japo mara zote huwa kuna gharama zake. 

Kwa hiyo kukiwa na mfumo mbaya wa uongozi katika Taifa uwe na uhakika kuwa hali hiyo hukubaliwa  na wananchi wenyewe. Na ukiona nchi inaendelea na kustawi basi ujue wananchi wake ndiyo sababu wa kutokea hayo mazuri unayoyaona. 

Nimekuwa nikimsikiliza Rais wa marekani mwenye asili ya Afrika, Barrack Obama. Mara kadhaa amekuwa akisema, hatua au mafanikio waliyoyapata Wamarekani yameletwa na Wamarekani wenyewe. Lakini hapa kwetu Tanzania, kwa mfano; unaweza kumsikia kiongozi akitamka wazi tena hadharani kuwa, maendeleo yameletwa na chama chake. 

Kwa mtu mwelewa, tayari unapata picha ya aina ya viongozi mlio nao. Kwangu mimi kusema, ‘maendeleo ya watanzania yameletwa na chama fulani’ ni kuwadharau wananchi. Maana nitajiuliza kama chama hicho ndiyo kimeleta maendeleo, wananchi walikuwa wapi na wanafanya nini? Siku zote maendeleo ya nchi huletwa na wananchi wenyewe. 

0 comments:

Post a Comment